WADAU WAZIDI KUMUUNGA MKONO RC MAKONDA UJENZI OFISI ZA WALIMU


Posted On: September 2nd, 2017
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe.Paul Makonda leo amekutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Wamiliki wa Malori ya Usafirishaji wa Mchanga ambao wamemuunga mkono kwenye kampeni ya Ujenzi wa Ofisi za Walimu kwa kujitolea kusafirisha mchanga wote utakaohitajika.
Wamiliki hao kwa kauli moja wamemwambia Makonda kuwa suala la kusafirisha mchanga wa kujenga Ofisi zote 402 watalibeba hao hivyo yeye aendelee na majukumu mengine.
Makonda ameshukuru Chama hicho kwa kutambua thamani na mchango wa mwalimu.
Amesema Walimu wakiboreshewa Mazingira ya kufanyia kazi itawawezesha kufanya kazi yao kwa ufanisi na kuwapatia wanafunzi Elimu bora itakayosaidia Taifa kuwa na wataalamu wa kutosha na kupunguza utegemezi wa wataalamu kutoka Nje ya Nchi.
Ametoa wito kwa Jamii kuendelea kuchangia Kampeni ya ujenzi wa Ofisi za Walimu ili Walimu wasifanyekazi kwenye mazingira Magumu.
Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Malori ya Kusafirisha Mchanga Bwana Emmanuel Moshi amesema kuwa wameamua kuunga mkono kutokana na juhudi za Makonda na kutambua thamani ya Mwalimu huku akieleza kuwa wataendelea kumuunga mkono.