RC MAKONDA: NIMEDHAMIRIA KUBORESHA MAZINGIRA YA ELIMU

Posted on: August 1st, 2017
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mheshimiwa Paul Makonda leo ameelezea Dhamira yake ya kuhakikisha ujenzi wa Ofisi za kisasa 402 za walimu pamoja na Vyoo kwa shule za Msingi na Sekondari zilizobainika kuwa upungufu wa huduma hizo.
Ofisi hizo za kisasa zitakuwa na sehemu ya Chumba cha Mwalimu Mkuu,Chumba cha Muhasibu, Chumba cha Katibu Muktasi pamoja na ofisi za Msaidizi wa Mwalimu mkuu na walimu wote huku zikiwa na Vyoo vya kisasa pamoja na Bafu.
"Siwezi kuwa na amani kama walimu wangu hawana ofisi wala vyoo katika shule 402, ni aibu na fedheha kwa walimu kugombania choo na mwanafunzi au kutumia vyoo vya majirani au Bar, hii sio heshima ya mwalimu wa Mkoa wangu,ndio maana nimeamua kuanza kufanyia kazi changamoto hizi," Alisema Makonda.
Kutokana na gharama za ujenzi kuwa kubwa Mheshimiwa Makonda ameviomba vyombo vya Ulinzi na usalama vya Mkoa wa Dar es Salaam kumpatia mafundi wa ujenzi kama sehemu ya kuunga mkono jitiada alizoanzisha za ujenzi wa Ofisi hizo ambapo vyombo hivyo vimeridhia kumuunga mkono.
“Kipekee napenda kuvipongeza vyombo vyote ya Ulinzi vilivyoamua kuniunga mkono vikiongozwa na Mkuu wa JKT kwa utayari wa kunipa vijana watakaofanya ujenzi huo, na niwaeleze kuwa ujenzi utaanza baada ya wiki mbili zijazo” Aliongeza Makonda.
Ujenzi wa Ofisi hizo unategemea zaidi jitiada za wadau wa maendeleo ikiwemo wamiliki wa kampuni pamoja na Wananchi wenye dhamira ya kuona Walimu wanafanya kazi katika mazingira Mazuri.
Tayari jitiada za Mheshimiwa Makonda zimeanza kuzaa matunda baada ya kufanikiwa kupata Mabati 11,000 na mifuko ya Saruji 1,000 ambapo Mahitaji ni Mabati 50,000/= Mbao zaidi ya Million mbili pamoja na vifaa vingine vya ujenzi.
Makonda amesema ataanza kutembelea viwanda vinavyojihusisha na uzalishaji wa vifaa vya ujenzi ikiwemo Mabati, Saruji, Nondo na vinginevyo kuona namna wanavyoweza kuunga mkono ujenzi huo ili kuhakikisha walimu wanafanya kazi katika mazingira rafiki.