CHANGAMOTO ZA HUDUMA YA AFYA NA WAGOMBEA URAIS KENYA
Suala la afya katika uchaguzi mkuu wa Kenya limekuwa likizungumziwa sana katika mikutano ya kampeni ya wagombea wakuu wa urais.
Mgombea wa jubilee Rais wa sasa Uhuru Kenyatta na kiongozi wa
muungano wa upinzani NASA, Raila Odinga wanatumia kila mbinu kusaka kura
za wakenya kwa kuwaahidi kuwa kipaumbele kitakuwa ni kuboresha sekta
hiyo ili wananchi wa Kenya wapate huduma bora za afya.
Ahadi kama hizo zilitolewa katika uchaguzi uliopita nchini humo
lakini hali ilikwenda kinyume pale madaktari wa Kenya na wauguzi
walipoanza mgomo mwaka jana kwa nyakati tofauti hadi mwaka huu.
Mwezi Januari rais Uhuru Kenyata alivunja ukimya wake na kuwataka madaktari kurudi kazini na kuruhusu mazungumzo kuendelea.
Zaidi ya madaktari 5,000 katika hospitali za umma walikuwa wanataka
serikali iwahakikishie mazingira bora kazini na nyongeza ya mshahara kwa
asilimia 300.
Serikali na wawakilishi wa madaktari walitia saini makubaliano ya
nyongeza ya mshahara na maswala mengine yaliyokuwa na mzozo alisema hayo
katibu mkuu wa jumuiya ya madaktari , mfamasia na mtaalamu wa meno,
bwana Ouma Oluga.
Madaktari wa hospitali za umma nchini Kenya waliopitia mafunzo ya
miaka sita katika vyuo vikuu wanalipwa kati ya $ dola 400 hadi 850 kwa
mwezi.
Sasa wakenya wakiwa wanahesabu siku kabla ya kutekeleza haki yao ya
kidemokrasia kumchagua rais atakayeongoza taifa hilo katika muhula ujao,
suala la afya limeangaliwa na kuzungumziwa kwa upana katika ulingo wa
siasa kwenye kipindi hichi cha kusaka kura katika uchaguzi mkuu. Rais
Uhuru Kenyatta anatoa ahadi tena kabla ya uchaguzi mkuu Agosti 8 mwaka
huu.
“Utawala wangu utahakikisha huduma za afya za msingi zinatolewa
bure, na wanawake wajawazito watahudumiwa wakati wote wa ujauzito hadi
pale watakapojifungua ikiwa ni miezi 12 ya huduma ya bure,” anasema rais
Kenyatta.
Anasema ameshuhudia wakenya wengi wakiuza mashamba na mali zao ili waweze kumudu huduma za afya sasa hilo halitakuwepo.
Kwa upande wake mgombea urais wa muungano wa NASA, Raila Odinga ameahidi kwamba matatizo ya afya yatatatuliwa kwa haraka.
“Jambo la kwanza ni kuunda tume ya huduma za afya ili makdaktari na
wauguzi wawe na fursa ya kufanya mashauriano ili masuala ya malipo yao
yaweze kushughulikiwa kwa njia ya mjadiliano zaidi, “ anasema.
Anasema endapo atakuwa kiongozi wa taifa hilo atahakikisha suala
linawasilishwa bungeni lijadiliwe na kuhakikisha tume huru ya huduma za
afya inaundwa
Wapiga kura wanasubiri kwa hamu kubwa kuona endapo atakayechaguliwa
atakuwa mwepesi kutekeleza yale aliyoahidi wakichukulia mfano wa kampeni
za miaka iliyopita na ahadi zake zilivyokuwa.
Post a Comment