Waziri Simbachawene ajiuzulu

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,- TAMISEMI, George Simbachawene
Responsive image
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,- TAMISEMI, George Simbachawene amejiuzulu wadhifa wake.
Simbachawene ametangaza uamuzi huo katika mkutano na waandishi wa habari mjini Dodoma na kumshukuru Rais kwa kumwamini na kumpa majukumu ambayo ameyafanya kwa kadri ya uwezo wake.
Aidha amewashukuru wananchi wa jimbo la Kibakwe waliomchagua na kumwezesha kuwa mbunge kabla ya kuteuliwa kuwa Waziri na hivyo kuahidi kuendelea kuwatumikia kwa moyo wake wote.
Hata hivyo Simbachawene amefikia uamuzi wa kuachia ngazi ya uwaziri ikiwa ni kuheshimu ushauri wa kamati zilizoundwa kuchunguza madini ya almasi na tanzanite iliyowasilishwa bungeni jana na kukabidhiwa kwa Rais Magufuli mapema leo.
Akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo Rais Magufuli ameagiza vyombo vya ulinzi vianze kazi mara moja kushughulikia suala hilo huku akiwataka wateule wake waliotajwa katika taarifa hizo kukaa pembeni kupisha uchunguzi.