'MTOTO WA NYANI' KIZIMBANI KWA UBAKAJI



KIJANA  aliyeishi na nyani tangu alipozaliwa baada ya kutupwa msituni mkoani shanyanga, amefikishwa mahakamani kwa makosa mawili, likiwemo la kubaka.

Baraka Joshua, maarufu kwa jina la mtoto wa nyani, alipandishwa kizimbani jana, katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, mbele ya Hakimu Mkazi Catherine Kiyoja.

Akimsomea mashitaka hayo, Wakili wa Serikali, Florida Wenceslaus, alidai Mei 17, mwaka huu, eneo la shule ya msingi Tabata Kimanga, mshitakiwa alimlawiti mtoto mwenye umri wa miaka tisa (jina linaifadhiwa).

Florida alidai katika shitaka la pili, siku hiyo hiyo mshitakiwa alimbaka mtoto huyo, ambaye alikuwa anasoma katika shule ya Kimanga.

Mshitakiwa alikana mashitaka yote mawili na kurudishwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.

Hakimu Catherine aliyataja masharti ya kuwa ni wadhamini wawili,
kati yao mmoja awe mtumishi wa serikali, watakaotia saini dhamana ya sh. milioni mbili kila mmoja.

Kesi hiyo itatajwa Mei 26, mwaka huu.
 
Katika maisha yake ya utotoni, mshitakiwa alikuwa akiishi na nyani porini kabla ya kuchukuliwa na watu wa maliasili baada ya kumfuatilia kwa karibu.

Imeelezwa kuwa mshitakiwa alipochukuliwa na maofisa wa idara hiyo, alifikishwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kuanza kutibiwa huku akifundishwa namna ya kutembea.

Kabla ya kupatiwa tiba na mafunzo hayo, mshitakiwa alikuwa amezoea maisha ya kinyani, ambapo alikuwa anatembea kama mnyama huyo, kuongea kwa sauti zao na kudandia miti.

Baada ya kutibiwa, alitokea msamaria mwema mmoja, ambaye alimchukua na kuishi naye, aliyemfungulia biashara ndogo katika maeneo ya shule ya msingi Kimanga.