Kenyatta atangaza vita kamili na al-Shabaab


Wapiganaji wa al-Shabaab wakionyesha silaha zao
Rais Uhuru Kenyatta ametangaza operesheni kabambe ya kuwamaliza al-Shabaab.
Akizungumza Jumatatu huko Kizingitini, Kaunti ya Lamu, Rais ameagiza kuwa magaidi wauawe na kuzikwa.
“Tutawamaliza magaidi wote,” amesema kwani magaidi hao wameugeuza msitu wa Boni ni mahali pa mchezo mchafu, ambapo wamekuwa wakiwashambulia na kuua wakazi wa eneo hilo kabla ya kutokomea katika msitu huo.
Vyanzo vya habari nchini Kenya vimesema Rais ambaye alionekana akiwa na hasira katika hotuba yake ambayo iliashiria pia kuwa kutekwa nyara Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Mariam El Maawy na magaidi hao wiki iliopita, na kupigwa risasi na kujeruhiwa, inawezekana alilengwa kwa sababu ya kutoa hati kwa wananchi wa eneo hilo.
Maawy aliokolewa na Jeshi la Ulinzi la Kenya baada ya wapiganaji hao wa al-Shabaab kuteka gari yake kabla ya kumuua mlinzi wake, dereva na mpwa wake. Watu wengine wawili walipoteza maisha katika tukio hilo.