Jeshi la polisi latangaza oparesheni maalumu ya kuwabaini wezi wa vifaa vya magari.

Jeshi la polisi kanda maalum ya dar es salaam limetangaza operesheni maalum ya kuwabaini wezi wa vifaa vya magari ambapo wafanyabiashara wote ambao wanauza vipuri vya magari vilivyotumika wanatakiwa kuonyesha nyaraka za kuingiza bidhaa zao hapa nchini pamoja na risiti za kodi walizolipia kodi na kama watashindwa kufanya hivyo wataunganishwa na kundi na wezi wa vifaa vya magari.

 Operesheni hiyo imetangazwa na kaimu kamanda wa polisi wa kanda hiyo Lucas Mkondya wakati akitangaza operesheni hiyo kwa umma ambapo amesema maduka mengi ya vifaa vya magari vimekuwa vikitumika kama sehemu ya kuuzia vitu vya wizi.


Aidha kamanda huyo amesema watahakikisha wanakomesha mtandao wote wa wezi wa magari na tayari wametuma kikosi maalaum cha polisi nje ya nchi kwenda kubaini mtandao huo wawezi wa magari.
Baadhi ya wananchi  wamepongeza mpango wa kuwabana wezi wa vifaa vya magari kwani wizi huo umekuwa sugu na watu wamekuwa wakiishi bila ya kuwa amani na magari yao.
Vilevile Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limefanikiwa kukamata silaha moja aina ya Shotgun ikiwa na risasi tano ndani ya magazine maeneo ya Pemba Mnazi wilaya ya Kigamboni Jijini humo.

Kamanda Lucas Mkondya ameeleza kuwa mnamo tarehe 16 Julai walikuta silaha hiyo yenye namba za usajili TZ CAR 3421  ikiwa imetelekezwa na watu wasiojulikana katika maeneo ya ufukwe wa bahari ya hindi wakati askari wakiwa doria, ambapo silaha hiyo imehifadhiwa kituo cha polisi Kigamboni na upelelezi unaendelea.
 
 
Katika Matukio mengine Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam Lucas Mkondya ameeleza kuwa mnamo tarehe 11 Julai mwaka huu limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa watatu kwa wizi wa magari huko Ukonga akiwemo Adamu Hamisi dereva na mkazi wa Kwamkolemba Moshi Bar Ukonga, Adamu Karubya-Dereva na Mkazi wa Vingunguti, na George Andrew  wakiwa na magari mawili ya wizi.

Magari hayo yaliyokamatwa ni pamoja na lenye namba za usajili T.730 CTJ aina ya Toyota Rav 4 rangi ya blue ambayo imefutwa Chasis namba, lingine ni gari namba T.212 DEF Toyota IST rangi nyeusi ambayo iliibiwa mnamo tarehe 1 mwezi wa  5 huko kipunguni Moshi Bar.

Aidha gari ya aina ya Toyota IST lilikamatwa huko Magomeni likiwa tayari kubadilishwa rangi yake ya awali ili kuwa na rangi nyeupe ikiwa pamoja na kubandikwa namba nyingine T.827 BZL.