Jafo alia siri za serikali kuvuja

Naibu Waziri ofisi ya Rais Tawala za mikoa na serikali za mitaa, Selemani Jafo ameonyesha kusikitishwa na kitendo cha siri za serikali kuvuja kwa watu na kusema hayo yote hutokea kutokana na watumishi wa serikali kutokuwa na siri.
Naibu Waziri ofisi ya Rais Tawala za mikoa na serikali za mitaa, Selemani Jafo.
Jafo amesema hayo leo wakati akifungua mafunzo ya uongozi kwa Wakuu wa wilaya na Wakurugenzi mbalimbali wa halmshauri mkutano ambao umefanyika makao makuu ya mji Dodoma, katika mafunzo hayo viongozi hao watafunza mambo mbalimbali ikiwepo kutunza siri za serikali, maadili ya uongozi na itifaki mbalimbali.
"Leo hii nchi yetu utakuja kuona kwa mfano Kamati ya ulinzi na usalama imejadili jambo fulani la siri kubwa sana kesho na kesho kutwa utakuja kuona siri hiyo ipo kwenye mtandao wa jamii imeshapostiwa habari mliyojadili ya siri kubwa sana lakini unakuta jambo hilo limeshatoka nje, leo hii nyaraka za serikali unaweza kumkuta mtu sehemu anazizungumza na kwamba kuna kikao fulani kilifanya jambo fulani nyaraka hiyo ilitokaje? Maanake kuna watu wanashindwa kutimiza majukumu yao katika utunzaji wa nyaraka za serikali na siri za serikali" alisisitiza Jafo 
Naibu Waziri aliendelea kuzungumza kuwa "Leo hii Mkurugenzi katika ofisi yako utakuta habari nyeti za ofisi yako zipo mtaani zinajadiliwa ambazo ukiangalia hali siyo salama kabisaa, jamanii siri ndiyo msingi unaosimamisha jambo lolote linalosimamisha muhimili" 
Mbali na hilo Jafo aliwataka Wakuu hao wa wilaya pamoja na Wakurugenzi hao kupambana na madawa ya kulevya, lakini pia amewataka kwenda kusimamia nidhamu ya watumishi wa umma na kuwataka wao wenyewe kuwa mfano wa kuwa na nidhamu nzuri katika utendaji wao wa kazi. Pia Naibu Waziri amewataka viongozi hao kwenda kusimamia amani na utulivu kwenye maeneo yao pamoja na kutatua migogoro mbalimbali ya ardhi.